Tuesday, June 30, 2009

TUNAFIKIRI VIZURI NA KWA WEPESI KATIKA LUGHA TUNAYOJUA VIZURI ZAIDI



Serikali inavyoua lugha za asili Tanzania
•Sera zake zina sura ya ‘ndumia kuwili’

Na Ndimara Tegambwage

SERIKALI ina tabia ya “ndumila kuwili” kuhusu nafasi ya lugha za asili. Inaonekana ina utashi wa kuua lugha hizo kwa madai ya kukuza Kiswahili.

Katika Sera ya Utamaduni ya mwaka 1997 serikali inasema, “Jamii zetu zitaendelea kutumia na kujivunia lugha zake za asili kwa kuwa ndio hazina kuu ya utamaduni na maarifa.”

Lakini katika Sera ya Habari ya mwaka 2003, serikali hiyohiyo inasema, “Lugha zitakazotumiwa na vyombo vya habari hapa nchini ni Kiswahili na Kiingereza.”

Katika sera moja serikali inatambua kuwepo utamaduni na maarifa katika lugha za asili; katika sera nyingine serikali inasema hizo lugha zilizosheheni maarifa, zisitumiwe kwenye vyombo vya habari.

Huu ni mpango wa kunyonga lugha za asili kwa kuzinyima pumzi – zisijitokeza kwenye vyombo vya kisasa vya mawasiliano mapana na hivyo kuteketeza hazina kuu ya utamaduni na maarifa.

Utamaduni na maarifa ni mazao ya akili. Ni matunda ya watu wanaofikiri na kutenda. Kinachoitwa hazina ya utamaduni ni mkusanyiko wa fikra na matendo ya watu katika jamii; katika kipindi maalum cha maisha yao.

Katika maana yake halisi, maarifa ni sehemu ya utamaduni pale tunapoainisha utamaduni kuwa ujumla wa maisha ya watu na mazingira yao katika jamii husika.

Sasa kwa nini maisha ya watu wengi, walioko katika mila, desturi na maarifa yao, yawekwe kando katika matumizi ya vyombo vya habari?

Huu ni ubaguzi wa aina yake, wenye sura ya unyanyapaa kwa mamilioni ya watu wasiozungumza Kiswahili wala Kiingereza.

Kuzuia matumizi ya lugha za asili kwenye mikutano na katika vyombo vya habari, ni ubaguzi wenye madhara yafuatayo:

Kwanza, ni kutaka kuua lugha husika. Ni kuua utamaduni na maarifa yaliyomo ambayo yalipatikana na yanaendelea kupatikana kupitia lugha hizo.

Maarifa hayo, ama yanaendelea kuundwa, yapo na yalikuwa hayajafahamika kwa mapana na, au hayakuwa yamesambazwa wala kuhifadhiwa katika lugha nyingine.

Pili, kunyang’anya wanaotumia lugha za asili uwezo wa kuelewa, kubaini na kushiriki maongezi na mijadala inayowahusu.

Tatu, kupandikiza utatanishi, woga na kutojiamini miongoni mwa wanaotumia lugha za asili. Hali hii inaletwa na shinikizo la kila mmoja kutumia lugha ya shuruti.

Nne, kuondoa mfumo na mtiririko wa kufikiri ambao watumiaji wa lugha za asili walikuwa wamezoea.

Tano, kupunguza, kuzuia au kufuta kabisa, mawasiliano mapana, kwa njia ya lugha na vitendo na hivyo kudumaza au kufisha maarifa katika jamii husika kwa kupunguza au kuondoa uwezo wa kuzalisha mawazo mapya.

Sita, kupunguza wepesi wa kufikiri na kuelewa na kuondoa mshikamano wa jamii zinazotumia lugha za asili.

Saba, kuvunja haki za binadamu kwa kuingilia, kutibua, kudhibiti, kukandamiza na kuzima lugha za asili – ambazo ni chombo cha fikra na maarifa kwa jamii husika.

Uvujaji huu wa haki za binadamu umechukua sura ya kuhujumu:

Kwanza, uhuru wa “kuwa wewe” na kuwa sehemu ya jamii yako kwanza kabla ya kuwa sehemu ya jamii pana.

Pili, uhuru wa kufikiri; tena kufikiri kwa wepesi na mtiririko. Tatu, uhuru wa kuwa na mawazo na kutoa na kupokea mawazo ya wengine. Nne, uhuru wa kutofautiana na mwenzako au yeyote; hata kama ni mtawala. Tano, uhuru wa kurithishana utamaduni na maarifa.

Lakini watawala, ambao pia ni watunga sera zinazogongana, wamekuwa wakidai kuwa lugha za asili zinawagawa Watanzania. Wanataka Kiswahili na Kiingereza tu.

Inabidi uwe mwendawazimu wa kiwango fulani ili uweze kuwasomea Wasukuma au Wamasai, wasiojua Kiswahili au Kiingereza, taarifa za habari za vijijini mwao, taifa au za kimataifa na kudai kuwa kwa njia hiyo unaunganisha taifa!
Nimepata fursa ya kuhudhuria warsha ya 10 ya Mradi wa Lugha za Tanzania (19 -20 Juni 2009), juu ya “Nafasi ya lugha za asili katika jamii ya Tanzania,” ukumbi wa hoteli ya Beachcomber nje ya jijini la Dar es Salaam.

Wachunguzi walikuwa wakionyesha, pamoja na mambo mengine, kazi walizochapisha juu ya lugha za watu wa jamii mbalimbali na kudhihirisha kuwa lugha ya kwanza kwa wananchi wengi, siyo Kiswahili.

Hoja hii inakuja kufuatia matokeo ya tafiti nyingi duniani kuwa watoto wakifundishwa katika lugha yao ya kwanza ambayo walimu wao wanaijua vema, angalau kwa madarasa ya awali, hupata uwezo wa kuelewa haraka na hata kupata msingi wa kushika lugha na masomo mengine.

Kama ada, takwimu za aina hiyo lazima zilete mgongano kati ya watetetezi wa lugha za asili na wale wanaopenda Kiswahili na Kiingereza hata kwa mgongo wa kifo cha lugha za asili.

Kuna wasomi waliosema lugha za asili hazina maana na kwamba hakuna maarifa yoyote ya kuchota kutoka kwa watumiaji wa lugha hizo (!)

Pamoja na kwamba wenye kutumia lugha za asili ni wengi na bado wanafikiri na kutenda katika lugha hizo kuliko Kiswahili na Kiingereza; kuna waliosema lugha hizo zimepitwa na wakati; zinyofolewe baadhi ya misamiati na istilahi na kuachwa zife.

Bali hoja kuu inabaki bila kujibiwa: Mbona kuna kasi, mabavu ya sera za serikali na mpogoko wa hoja za baadhi ya wasomi katika kuhujumu lugha za asili?

Tatizo basi siyo kwamba lugha za asili zinawagawa Watanzania. Tatizo ni kwamba wananchi wakiendelea kuwasiliana katika lugha zao, ambamo wanaelewana vizuri na kutenda kwa muwafaka, yafuatayo yatadhihiri:

Kwanza, watafikiri, tena kwa wepesi na kuelewana vizuri. Pili, wataungana zaidi na kuwa na mshikamano zaidi. Tatu, watasimamia utashi na kauli zao na hata kuvunja mikatale iliyowafunga miaka nendarudi.

Kwa msingi huu, malalamiko ya watawala kuwa lugha za asili zinagawa wananchi, na kuchochea ukabila, yanalenga kuhujumu uwezo huo wa kufikiri na kutenda kwa uhuru.

Suala la ukabila bado limo katika vichwa vya wasomi wengi wenye vyeti vya hadhi ya juu katika taaluma mbalimbali. Huu nao ni msiba. Bado kuna wanaofikiri kuwa kuongea Luhaya au lugha yoyote ile ya asili, ni kuwa na ukabila.

Hawa hawajui au wamesahahu au wanakataa kukubali kuwa mtu anafikiri haraka katika lugha yake ya karibu zaidi; mifano yake inakuja haraka kupitia lugha hiyo; anakuwa mwepesi kuwasilisha na kutoa majibu katika lugha yake na hasa anapokuwa anaongea na wanaofahamu lugha yake.

Hata baadhi ya wasomi vyuoni bado wana matatizo na Kiswahili na Kiingereza. Sharti wafikiri kwanza, kwa mfano kwa Luhaya, ndipo waweke kwenye Kiswahili na baadaye watoe sauti kwa Kiingereza.

Watu hufikiri vizuri na kwa usahihi zaidi katika lugha zao na hii ni haki yao kama walivyo na haki ya kuishi. Bali watawala na wengine waliomezwa na mkengeuko wameng’ang’ania dhana dhaifu kuwa lugha za asili zinaligawa taifa.

Je, tumekuwa na makabila au nchi au mataifa madogo? Twende Bukoba. Tarehe 8 Julai 1931, Omwami Rwagugira alikabidhiwa nishani aliyopewa na King George wa Uingereza (usijali sababu).

Katika hotuba yake ya kukabidhi nishani, Bwana PC (mtawala wa jimbo – Provincial Commissioner) alisema, “Mwami Rwamugira amepewa nishani kwa uhodari wake na kazi alizofanya toka sisi tumeingia katika nchi hii ya Bukoba…”

Tarehe 28 Mei 1933, Omukama wa Ihangiro alikaribisha masultani kutoka Dar es Salaam kwa kusema, “…Sina budi kutoa shukrani kwa watemi hawa waliofika katika mji wangu wa Rubungo na nchi yangu ya Ihangiro…” (Kutoka:Kitabu ya barua kakobi, 1931).

Kwa ufupi, hapa kulikuwa na watu. Wana utawala wao na lugha yao katika taifa lao. Waliongea, kufikiri na kutenda katika lugha yao.

Wageni, kama Bw. PC na masultani walipata wakalimani na kumbukumbu ziliwekwa; tofauti kabisa na ubwege wa sasa ambako mzungu mmoja anafanya warsha ya wananchi 60 kuendeshwa kwa lugha ya Kiingereza.

Kauli hizi za Bakama kuhusu “nchi zao” hazikuja na ukoloni wa Uingereza. Wakoloni walizikuta na hali yake halisi. Kumbuka hiyo ni miaka 47 tangu Afrika ikatwe vipande kama keki ya harusi (1884).

Historia imejaa kumbukumbu, siyo tu za Tanganyika, ambako walitangulia Wajerumani na kabla ya hapo Waarabu, bali Afrika nzima inaonyesha kuwepo kwa tawala imara, zikiwa mataifa kamili, hata kama hazikuwa na silaha kama za wavamizi.

Vita vya kupambana na wavamizi Afrika viliendeshwa na viongozi wa mataifa ya Afrika yaliyokuwa yameimarika katika tawala zake. Ujio wa teknolojia mpya hauondoi ukweli wa utaifa.

Historia imejaa orodha ya watawala na viongozi wa vita walionyongwa au waliojiua kuliko kuchukuliwa mateka na wavamizi. Mapambano yote hayo yaliendeshwa katika lugha za asili zilizolingana na maendeleo ya teknolojia ya wakati huo.

Kitu kikubwa kiliwashinda wavamizi wote katika historia. Walishindwa kuua lugha walizozikuta. Ukinzani kati ya makundi mawili ya “kigaidi” – wamisionari na wakoloni – ulizaa mbegu moja ambayo haikuwa imekusudiwa.

Wamisionari walishikilia baadhi ya lugha za asili na kuandika na kutafsiri vitabu vya dini katika lugha za wenyeji.

Hawa walijua “neno halitapenya” kwa lugha ya mbali. Halitazungumzwa baada ya mahubiri. Halitakaa moyoni kama halina mfano wa karibu. Halitakumbukwa kama halikuwekwa katika mvumo unaoeleweka na uliozoeleka.

Kama kuna kitu kimoja tunachoweza kujivunia kwa kushinda uvamizi uliofanywa Afrika, ni kubakiwa na lugha za asili zilizosheheni maarifa ya jamii mbalimbali.

Ndani yake kumefunikwa upendo na mshikamano wa jamii; chuki na hasira dhidi ya wavamizi; mbinu za kujikinga na kuendelea kuishi; ujasiri wa kukabiliana na adui; hekima ya kufanyia maamuzi; maarifa ya kuendeleza jamii na fursa za kuingizia maarifa mapya.

Kwa hiyo, hapa kulikuwa na tawala, siyo makabila wala vikabila. Kulikuwa na lugha za mataifa zilizohudumia jamii anuwai katika kila nyanja.

Ndani ya kitabu cha nyimbo za Luhaya za Kanisa la Kilutheri cha hadi miaka ya 1950 kulikuwa na wimbo uliotungwa kwa msingi wa kizalendo na kwa mantiki zote ulikuwa wimbo wa taifa:

Mukama Katonda linda
Eihanga lya Buhaya
Abantu n’eitunga lyamwo
Ensi ogihe omugisha
Linda amaju n’ebibanja
Endimilo ozezege
Nabo abantu bakusiime
Bakuhulile wenka


Tafsiri ya karibu ni:
Ee Baba Muumba
Dumisha taifa la Buhaya
Watu na mali zao
Nchi uipe neema
Linda kaya na mashamba
Mavuno yawe teletele
Ndipo watu wakuhimidi
Na kukutii wewe tu


Kanisa lilitambua utaifa wa mataifa mengi lakini katika lugha zao. Angalia jinsi ubeti wa wimbo uleule ulivyobadilishwa kukidhi maendeleo ya kisiasa (chapisho jipya):

Mukama Katonda linda
Ensi ya Tanzania
Naichwe abantu otulinde
Ensi ogihe omugisha
Kandi abemiluka yoona
Obahe obwesigwa
Singa waitu otubele
Chwena tukuhulile

(Kutoka: Empoya, Northwestern Publishers, 1992)

Tafsiri ya karibu:
Ee Baba Muumba
Dumisha taifa la Tanzania
Nasi watu utukinge
Nchi uipe neema
Na wote wenye majukumu
Uwape uadilifu
Eee Mungu utuwezeshe
Sote tukutii wewe


Pamoja na mabadiliko kutoka taifa la Buhaya kwenda taifa la Tanzania, bado nafasi ya lugha ya asili ni muhimu kuelezea kilichotokea ili kieleweke vema kwa wengi, kijadiliwe, kizame na watumiaji wa lugha hiyo waweze kufuatilia na kupima mabadiliko.

Hivyo, kuzima lugha za asili kunalenga kuweka kando wananchi waliopevuka ndani ya lugha zao na kufanya jamii zenye uelewa mpana kupitia lugha za asili, kuwa kama misukule ya kuswagwa bila utashi.

Kuhujumu lugha za asili ni kueneza ujinga. Watu hawatajua jinsi serikali ilivyoshindwa kutekeleza ahadi zake za kuondoa ujinga, umasikini, rushwa, magendo na ufisadi. Hivyo hawatachukua hatua.

Kwani watawala wana tabia ya kupakata umasikini na ujinga. Umasikini hufanya wengi kubaki hohehahe, tegemezi na hata ombaomba.

Ujinga hufanya wasijue na hasa mara hii wanapokuwa wanaelezwa kwa lugha ngeni, ngumu ambazo hawajui vema au hawajui kabisa na hawawezi kuzitumia kung’amua kinachoendelea. Kwa hiyo, ujinga na umasikini ni mtaji na ngao kuu za watawala.

Kwa upande mwingine, matumizi ya lugha za asili katika vyombo vya habari yangewezesha jamii pana kuelewa kinachojadiliwa; kuchangia na kukuza hoja na hata kuunga mkono au kukataa hoja.

Nani atashindwa kufarijika kwa kuona wenye ujuzi wa lugha za asili wakiajiriwa katika vyombo vya habari na serikali ikijitahidi kujua kilichomo kwa kuajiri wakalimani. Ajira.
Mbona umoja wa watu wenye lugha anuai na wanaoelewa umuhimu na shabaha yao, unaweza kuwa imara kuliko umoja wa kushinikiza kupitia lugha moja au na nyingine ya kigeni?

Bado Kiswahili kinaweza kuendelea kutumika na kukuzwa, kama kuna juhudi za kufanya hivyo. Bali kuwepo kwa lugha za asili, nyingi kama zilivyo, siyo tishio, ni fursa.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la MwanaHALISI,toleo la Jumatano, 1 Julai 2009)

SERIKALI IOMBE ASKARI WAKAE KIMYA


Mawe yakisema, serikali itaumbuka

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI waziri Jeremiah Sumari achokoze Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kwa kutumwa au kwa sababu zake binafsi.

Majeshi ni mawe makubwa. Majabali. Miamba. Majeshi ni wagumba. Majeshi yakitaka kuzaa sharti yakubali kufa polepole; kwa maana kwamba atokee wa kuyapasua ili yatoke mengi kwenye mawe makubwa au miamba. Hapo hayabaki mojamoja na imara tena.

Na kawaida majeshi ya nchi hayachokozwi na mtu wa ndani wala wa nje. Wachokozi huchokoza nchi na watawala wa nchi zilizochokozwa huagiza majeshi yake kwenda mstari wa mbele na kukunja uchokozi kama jamvi la wageni.

Lakini uchokozi uliofanywa na waziri Sumari ni wa ndani na unaweza kufanya mawe makubwa, miamba kutamani kutoa sauti na kusema hayataki kupasuliwa; yaachwe kama yalivyo.

Akijibu swali la Dk. Willibrod Slaa juu ya ufisadi ndani ya mradi wa Meremeta, Sumari alitoa majibu ya vitisho. Alimwambia mwakilishi wa Karatu (CHADEMA) aachane na hoja ya ufisadi ndani ya Meremeta.

Kiasi kinachodaiwa kupitia Meremeta kwenda mifuko isiyojulikana si haba. Ni zaidi ya Sh. 155 bilioni. Waziri anamwambia mbunge aachane na hoja ya Meremeta kwa madai kuwa mradi huo ulikuwa wa jeshi; kwamba ni suala nyeti na labda ni kuingilia suala la usalama wa taifa.

Waziri anataka kulazimisha mawe kusema. Mawe yatabaki kimya juu ya ahadi zao; juu ya mipango yao na silaha zao; juu ya mikakati ya sasa na baadaye; juu ya mbinu mpya walizopata katika medani ya vita; juu ya wanachopanga kufanya hivi sasa.

Ukimya huu ni kama jua, mvua na upepo vipigapo kwenye mwamba na mwamba ukavumilia. Zaidi ya hapo, miamba husema. Miamba mingi imeota juu ya mizimu ya kale iongeayo wakati wa jua kali.

Inawezekana, siku moja unapita karibu na miamba hiyo, wakati wa jua kali, ukasikia mtu akikuita kwa sauti ya juu sana – mara mbili au mara tatu – na usimwone.

Wale dhaifu wa moyo huweza kuanguka chini na kuzimia; wengine humudu kukimbia hadi nyumbani kwao, wakitweta na kulowa jasho mwili mzima huku wakiishiwa na kauli. Mawe, majabali, miamba imeamua kusema!

Wakati huo hujawahi kuichokoza. Hujailalamikia wala kuituhumu. Hujaisingizia wala kuihusisha katika miradi bubu ya watawala. Inasema tu. Inabubujika. Sembuse utakapoihusisha na wizi, uporaji, ukwapuaji, au kwa ujumla – ufisadi!

Ikae kimya? Sitaki waziri Sumari achokoze miamba na yenyewe iseme kwamba haijui Meremeta ni nini na ya nani. Kwamba haijawahi kunufaika na kampuni hiyo. Kwamba mafao yaliyotokana na Meremeta hayafahamiki jeshini. Kwamba hayakuingia jeshini.

Sitaki waziri achokoze miamba ianze kukohoa na kunong’ona na hatimaye kulipuka. Miamba hii inajua kuwa fedha za kuendesha jeshi hutoka kwenye bajeti ya serikali inayosomwa na kupitishwa bungeni.

Miamba hii inaelewa vema kwamba wakati Meremeta wanaanzisha mradi walihamisha wananchi kutoka makazi yao. Walihamisha hata kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa na kutawanya askari katika vijiji kwa kutumia mikokoteni.

Si wananchi – raia, wala askari walionufaika na mafao ya Maremeta baada ya kuanza kuvuna kutokana na mgodi. Shule na zahanati vilivyong’olewa havijarudishwa. Bwawa kubwa la maji lililokuwa sehemu ya uhai wa watu na viumbe anuwai, halijarejeshewa hadhi yake.

Sitaki watawala jeshini wajitokeze na kuiumbua serikali juu ya matumizi haya. Sitaki wapatikane watumishi wa Wizara ya Ulinzi na kuthibitisha kuwa hawajawahi kupanga fedha za Meremeta au sehemu yake katika matumizi ya wizara.

Sitaki maofisa wa ngazi za kati jeshi waanze kufurukuta na kusema hawataki kusingiziwa katika suala la ukwapuaji na hivyo kujitokeza na ukweli utakaoangamniza hadhi ndogo ya watawala iliyosalia.

Sitaki askari wa vyeo vya chini ambao wanajua vema kilichokuwa kinaendelea waanze kujitokeza na kusema walichoona na nani hasa walikuwa wavunaji wakuu wa Meremeta na siyo jeshi.

Wala sitaki askari wakumbushe serikali kwamba Tume ya Jaji Bomani iliishasema kuwa Meremeta si mali ya serikali bali ni ya binafsi. Labda likisemwa na wao ndipo serikali itasikia na waziri Sumari ataelewa.

Nani anataka azibuliwe masikio kuliko alivyofanya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Aliiambia Kamati ya Bunge kuwa Meremeta haimo katika orodha ya mashirika ya umma na kwamba ofisi yake haijawahi kuikagua.

Mei mwaka jana tulipeleka baruapepe kwa benki ya Nedcor Trade Services ya Afrika Kusini kuhusiana na suala hili. Hatukujibiwa. Tuliwaandikia Deutsche Bank AG ya Uingereza. Hawakujibu.

Lakini kwa kufuatilia kinachoendelea ni kwamba serikali haifanyi lolote. Imetafuta mahali pa kuegesha na kusahau hoja za wananchi wanaotaka kujua huyu Meremeta ni nani na fedha alizochota alizitumia wapi.

Matumizi ya visingizio vya jeshi, kama anavyosema Sumari, hayana uzito tena. Hayamtishi yeyote. Wananchi, wachunguzi na wengine wanaotafuta ukweli wangestuka na hata kuogopa kama wangekuwa wameingilia undani wa shughuli za jeshi.

Lakini hili la kikampuni cha Meremeta halimtishi mtu. Badala yake linaweza kuiweka serikali pabaya, kwani inaendelea kujichanganya; kuficha ukweli na hatimaye kusema uwongo.

Hatari kubwa inaweza kuzuka pale mawe, majabali na miamba itakaoamua kuvunja kimya; siyo lazima kwa mikutano ya hadhara bali kwa mn’ong’ono tu ambao hatimaye utavuma kama upepo wa kimbunga.

Na askari – hiyo miamba – ni watoto wa watu masikini na wao ni masikini pia. Hawana cha kupoteza kwa kusema ukweli wanaoujua. Hapo ndipo serikali itaumbuka zaidi.

Nani anaweza kuiondolea aibu serikali kwa kusema ukweli na kuijengea heshima na uhalali? Kama siyo mawaziri wake, nani hasa? Tusubiri majabali yaite wakati wa jua kali na kwa mzizimo wahusika wazimie?

Uwezekano wa aliyezimia kupitiliza hadi dunia nyingine ni mkubwa kuliko aliyesimama. Kwa nini serikali ijiingize kwenye majaribu tata? Ukimya unaidhalilisha serikali na kuiondolewa uhalali. Itoboe kilichomo ndani ya Meremeta.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hi ilichapishwa katika toleo la Jumapili, 28 Juni 2009 la
Tanzania Daima Jumapili)

Wednesday, June 17, 2009

BAJETI INAYOPIGA MIAYO




MJADALA WA BAJETI ULIOJAA VISINGIZIO

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI mjadala juu ya bajeti ya mwaka 2009/10 kwa kuwa tayari umezaa visingizio. Kwani iwapo bajeti itashindwa kukidhi matarajio, serikali itajitetea kwa kusema, “kulikuwa na hali mbaya ya uchumi duniani.”

Lakini bajeti hii ina somo kuu kwa walioko serikalini na maeneo mengine yanayohusiana na utawala kisiasa na kifedha. Kuna kila sababu kwa wahusika kuanza twisheni.

Siku moja kabla waziri wa Fedha na Uchumi kusoma bajeti bungeni, Rais Jakaya Kikwete alihutubia taifa. Alisema hali ya taifa si nzuri kiuchumi kutokana na msukosuko wa kiuchumi duniani. Akasema serikali imetenga Sh. 1.7 trilioni katika bajeti ya sasa kukabiliana na hali hiyo.

Lakini wananchi wanakumbuka kuwa, wakati taarifa zimeenea dunia nzima kuhusu kuanguka kwa uchumi wa mabepari-viongozi duniani, Gavana wa Benki Kuu (BoT) na mawaziri katika serikali ya Kikwete walinukuliwa wakisema “Tanzania haitaathirika” kutokana na hali hiyo.

Leo tunaambiwa Tanzania imeathirika na rais analazimika kuandika dibaji ya bajeti ya taifa, ikiwa njia ya kujenga hoja ya kuweka kibano katika kukusanya kodi ili kupata fedha za kujinusuru.

Je, gavana na mawaziri walipata wapi kauli hizo? Je, wana uelewa wa aina gani kuhusu mifumo ya fedha duniani? Je, wanajua mahusiano ya fedha za madola makubwa duniani na fedha za nchi hii? Maswali ni mengi.

Inawezekana watawala wa siasa na fedha hawakujifunza hili shuleni na vyuoni? Inawezekana walisoma zamani na sasa wamesahau na hivyo wanahitaji kukumbushwa kwa njia ya twisheni?

Labda watawala wa siasa na fedha walitaka kuficha kinachobisha hodi. Wahaya husema katika methali, “Ekyaizile mabele” – huwezi kuficha matiti ya msichana yaliyoanza kuchomoza. Yataonekana tu.”

Kuficha kumekuwa tabia ya viongozi. Hakuna mvua. Kuna ukame mkubwa na mazao yamekauka. Viongozi watasema, “Hakuna njaa na hakuna atakayekufa kwa njaa.”

Watu wanakabwa na kunyang’anywa walichonacho. Nyumba zinabomolewa usiku na mchana na vitu mbalimbali vinaibwa. Watoto wa kike wanabakwa, albino wanakatwa viungo vya mwili na wengine kuuawa. Wengi wanashinda na kulala njaa. Viongozi watasema nchi ni shwari na kuna amani na utulivu.

Sasa huu ni ugonjwa; na ukificha ugonjwa kifo kitakuumbua. Kile ambacho gavana wa BoT na mawaziri walikuwa wakidai hakipo, ndicho kinaingizwa kwenye bajeti.

Rais ambaye hakuwakemea wateule wake wakati wanatoa kauli zisizoweza kuthaminika katika medani ya uchumi wala siasa, leo analazimika kuwaambia wananchi kuwa na “uvumilivu” wakati wa utekelezaji wa bajeti ya kujikwamua.

Uchumi wa Tanzania utakosaje kuathirika kwa mafua ya uchumi wa nchi za kibeberu wakati ni sehemu yake? Uchumi tegemezi utakosaje kuathirika wakati anayetegemewa kayumba?

Uchumi usiokuwa na viwanda wala kilimo – zile injini kubwa; na ambao hata umeshindwa kunadi vivutio vya asili kwa njia ya utalii – tunajua nchi zinaoishi kwa utalii tu – utakosaje kuyumba na hata kuanguka?

Gavana na waziri wanaweza kushindwa vipi kuona kuwa kushuka kwa mapato katika nchi za kibeberu; kufilisika kwa viwanda, kuongezeka kwa idadi ya wasio na kazi na kupungua au kukosekana kwa huduma za jamii kwa wasio na kazi, vinaweza kuathiri uchumi wa Tanzania?

Kwani walipa kodi wakubwa katika serikali zinazotoa mikopo na misaada wakiishiwa, wakafilisika au hata wakilegalega, kwa nini serikali zao ziendelee kufikiria Tanzania? Watapunguza au watasitisha mikopo au misaada. Lazima nchi itaathirika.

Kama kauli za kutoathirika zilikuwa zinatolewa na wahusika ili kuficha janga na ili kuepusha “kuogopesha wananchi,” basi huu ni utoto wa ukubwani katika siasa na uchumi.

Watanzania wengi sasa wanajua kuwa wanaishi kwa mashaka kutokana na sababu nyingi. Watawala wake wameshindwa hata kukusanya na kuweka akiba ya chakula. Likitokea janga pana la miezi mitatu, tayari serikali itaanza kuhaha kutafuta chakula kutoka nje ya nchi.

Hapa twende kwa mfano mmoja tu wa pamba. Serikali ilikuwa inaendesha karibu viwanda 20 vya nguo. Ikashindwa kuviendesha. Vikafa. Sasa tunauza pamba nchi za nje. Viwanda vya nje vinavyotumia pamba vikikwama, basi pamba haitanunuliwa na iliyokusanywa itaozea ilipo.

Mkulima wa pamba asipouza pamba, hatalima tena. Asilipolima pamba na hana zao jingine, atafukarika zaidi, yeye na familia yake. Atakufa polepole. Kifo ndiyo hatima ya mahusiano kati ya Mtanzania na ubeberu.

Hili linaweza kuonekana vema zaidi katika mazingira ya sasa; na hii ndiyo hali halisi katika nchi zote zinazojiita “changa” hata baada ya nusu karne ya kutoka kwenye ukoloni.

Nchi zote ambazo zimebaki kuwa shamba la bibi, ambamo wenye viwanda wanachota malighafi – mazao na madini – kama wanavyotaka, lazima zikose usingizi hivi sasa.

Kwa hiyo, kwa jinsi mfumo wa sasa wa uchumi wa nchi hii ulivyoshonwa kwenye mfumo wa uchumi wa kibeberu, siyo rahisi kukwepa mstuko, msukosuko na hata kuanguka kabisa kwa uchumi na kuangamia kwa watu wake.

Labda baada ya hili kutakuwa na funzo.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii ilichapishwa katika toleo la Jumapili, 14 Juni 2007 la gazeti la Tanzania Daima Jumapili chini ya safu ya SITAKI)

MAMILIONI ZAIDI WATAKUFA KWA MALARIA




Ubeberu wanona kwa mgongo wa malaria

Na Ndimara Tegambwage

UHAI wa wananchi katika nchi za joto (tropiki), Tanzania ikiwemo, uko hatarini kutokana na ugonjwa wa malaria unaoua kwa wingi na kwa kasi kuliko ukimwi.

Nchi hizi, hasa watawala wake, wamejisahau. Badala ya kuchochea matumizi ya tiba asilia zilizoko kwenye makazi ya watu; na kuweka mazingira ya kujenga viwanda vyake, wameendelea kutegemea dawa kutoka viwanda vikubwa vya nje.

Matokeo ya uzembe huu wa kujisahau ni makubwa na mabaya. Watafiti wanaotoka nchi zenye viwanda vya dawa, wataendelea kupendekeza ni dawa ipi “bora” wamegundua itumike kutibu malaria.

Wakati huo wenye viwanda vya kutengeneza dawa na wafanyabiashara katika tasnia hii, wataendelea kutoa na kusimamia bei ya bidhaa hiyo bila kujali nani tajiri na nani masikini.

Kwa hiyo, kutokuwepo matumizi mapana ya dawa asilia; kutokuwepo utafiti na ujenzi wa viwanda vya ndani vya kutengeneza dawa; na kutokuwepo ruzuku kwenye dawa zinazotoka nje ili zipatikane bure au kwa bei inayowezekana, basi watu wengi watakufa kwa malaria.

Sasa serikali ya Tanzania imekiri kuwa bei ya dawa ya kutibu ugonjwa wa malaria, ambayo imeiidhinisha itumike, ni kubwa mno na wananchi hawawezi kuimudu.

Katika kipindi cha karibu miaka kumi, serikali imesema klorokwini (CQ) haifai, iachwe. Ikaachwa. Ikaleta SP (Sulphadoxine-pyrimethamine). Baadaye ikasema hata hiyo haifai, iachwe. Ikaachwa.

Serikali imekuja na dawa inayoitwa “mseto,” kwa ufupi wa ALU. Kabla hii haijaenea nchini, sasa inakiri kwamba imeleta kinyamkera. Dawa hii ni ghali sana. Dozi moja ni kati ya Sh. 13,000 na Sh. 15,000.

Hii maana yake ni nini? Ni kwamba Tanzania inashirikishwa, kwa kujua au kutojua, katika mchezo unaoangamiza maisha ya mamilioni ya wananchi na wakazi wengine katika nchi za tropiki, ambako ugonjwa wa malaria unaua bila simile.

Uchunguzi unaonyesha kuwa karibu watu milioni tatu hufa kwa malaria kila mwaka katika nchi za tropiki. Kati ya idadi hiyo, milioni moja ni watoto; ambayo maana yake ni kuwa mtoto mmoja hufa duniani kila baada ya sekunde 30.

Haya ni maafa makubwa na mbu aina ya Anofelesi, ambaye hueneza malaria, tayari amepewa na watafiti na walio katika mapambano dhidi ya malaria, jina la “gaidi mkubwa kuliko wote duniani.”

Gaidi huyu amenufaisha wenye viwanda vya kutengeneza dawa za kupambana na malaria na wote walio katika mkondo wa biashara ya dawa hizi, kiasi kwamba wagonjwa katika nchi masikini watakosa tiba. Watakufa.

Mkurugenzi wa Roche, kampuni kubwa ya kutengeneza dawa aliyeko Korea Kusini amenukuliwa akisema, “…Hatuko katika biashara ya kuokoa maisha ya watu, bali kupata fedha; uokoaji maisha siyo jukumu letu…”

Alikuwa akijibu ombi kwa kampuni yake kupunguza bei ya dawa za kukabiliana na ukimwi. Inatarajiwa atakuwa na kauli ileile au kali zaidi akiombwa kupunguza bei ya dawa za malaria kwa watu wanaoishi kwenye tropiki.

Katika hatua nyingine, mkondo mwingine wa viwanda, katika kasi isiyo ya kawaida, umetengeneza dawa bandia. Kwa hiyo, wakati dawa halisi haikamatiki kwa bei, dawa bandia haitibu au ni sumu.

Waziri wa Afya, Profesa David Mwakyusa alikiri jijini Dar es Salaam wiki iliyopita kuwa dawa ya malaria ambayo imependekezwa na wataalam, hainunuliki. Ni ghali sana.

Alirejea kilio cha mataifa masikini na wanaowaunga mkono, kuwa uundwe mfuko wa kimataifa (Global Fund) ambamo wenye fedha watachangia, ili fedha hizo zipelekwe kwa wenye viwanda vya dawa kupunguza gharama za uzalishaji na hivyo kupunguza bei ya dawa husika kwa watumiaji.

Hii ina maana “watu wema” wamchangie fedha tajiri mwenye viwanda vya kutengeneza dawa, ili apunguze gharama za uzalishaji na ili bei ya dawa ipungue.

Nchi masikini za tropiki zimeshindwa kupata mwelekeo katika kuzuia na kutibu malaria. Kwanza, zimeshindwa kuua mbu Anofelesi anayeeneza ugonjwa huu. Pili, zimeshindwa kupata tiba inayopatikana kwa gharama nafuu, kwa wepesi na karibu na makazi yao.

Kinachofanyika hivi sasa ni watawala kubabaika; kutapatapa na kuburuzwa na makampuni yanayotengeneza dawa za kutibu malaria.

Inawezekana hakuna kuburuzwa, bali watawala na makampuni kadhaa katika nchi hizi, wanashiriki biashara haramu ya “kuzalisha fedha” na siyo “kuokoa maisha” ya watu.

Kwa hiyo, likija pendekezo kuwa baada ya miaka 50 sasa “klorokwini” haimudu tena kutibu malaria, basi watawala na wataalam wa nchi hizi masikini, ama huchekea kiganjani kwa mtindo wa “kufa kufaana;” au huanza kuweweseka.

Rafiki yangu, Leonard Mutakyahwa, aishiye Dar es Salaam na Morogoro, hukumbwa na malaria kila baada ya miaka mitatu na nusu au minne. Lakini hadi hivi karibuni alikuwa akiendelea kutumia vidonge vya klorokwini kutibu malaria. Ilikuwa haijamkataa.

Mutakyahwa anaishi mjini. Lakini Mzee Flaviani Byeyombo wa kijiji cha Bushumba, Muleba ambako nilizaliwa na kukulia, hajawahi kumeza kidonge cha klorokwini au chochote kile cha kutibu malaria.

Mzee huyu hutumia mitishamba. “Kila nipatwapo na homa – mwili kukanyanyaa na kulegea, nikaumwa kichwa na wakati mwingine kuanza kuona kizunguzungu, macho kutoona vizuri na wakati mwingine kuwa na kichefuchefu, basi najua ndiyo hiyo mnayoita malaria imenitembelea,” anaeleza.

Maelezo ya Byeyombo hayaonyeshi dalili ya malaria peke yake. Dalili hizo zaweza kuwa za magonjwa mengine mengi.

Kwa hiyo dawa anayotumia mzee huyu, familia yake na wenzake kijijini, ni mseto wa majani ya miti mingi unaoitwa omubazi g’womushana kwa kutibu malaria na magonjwa mengi mengine na hata kuwa kirutubisho.

Hata Wahaya na wakazi wa muda mrefu wa Bukoba (Buhaya) ambao sasa wanaishi Dar es Salaam na miji mingine, na ambao wameendeleza mila na desturi za vyakula vyao na tiba, bado wanatumia mseto huu kwa tiba nyingi.

Unaweza kupendekeza bila woga, kwamba bila mitishamba, watu waishio katika nchi za tropiki wangekuwa wameteketea wote; kwani wanaofikiwa na vidonge vya kuzuia au kutibu malaria ni idadi ndogo – hasa Afrika.

Haya ndiyo maisha ya mamilioni ya watu waishio mijini. Kidonge au kijiko cha dawa ya kunywa kutuliza kikohozi, kuondoa mwasho mwilini, kuongeza damu; kukomesha kuhara au kutibu malaria, hakifiki mbali. Mitishamba ndiyo imekuwa ngao na tiba kuu.

Ukitaka waweza kusema kuwa wakazi wa nchi za tropiki waishio nje ya miji, wamejilinda, kujikinga na kujitibu kuliko tawala ambazo zinaweza kuwa zinakimbilia hongo ya asilimia 10 kwenye gharama ya dawa za viwandani; na nyingine zikiwa feki.

Hata kule ambako kidonge kama klorokwini kilipenya, matumizi yake hayakuwa sahihi. Kutokuwepo elimu ya kutosha juu ya matumizi, ama kulisababisha vifo au usugu wa malaria.

Nakumbuka Mama Zulfa, kijijini Bushumba, Muleba aliyenieleza mwaka 1996, “Nimechukua hivyo hapo (vidonge vya klorokwini); juzi nilimeza viwili, hivyo vingine viwili nitameza tena huko mbele iwapo nitajisikia homa tena.”

Katika kijiji cha Mwamihanza, Shinyanga, mwaka 1985, tukiwa kwenye ziara ya Mwalimu Julius Nyerere, mama mmoja aliniambia alivyonunua vidonge vinne vya klorokwini na kuwagawia watoto wake wanne – kila mmoja kidonge kimoja. “Naona sasa wanaendelea vizuri,” alieleza.

Kwa hiyo, klorokwini, SP na hata ALU, ni baadhi ya dawa ambazo zimekuwa zikibambikizwa kwa jamii hata bila maelezo ya kutosha kuhusu matumizi bora.

Kupungua kwa kinga dhidi ya malaria na usugu wa ugonjwa huo, haviwezi kamwe kuwa kwa viwango sawa kwa sehemu zote katika nchi moja au katika nchi zote za tropiki.

Bali hakuna anayetaka kujua ni sehemu gani ya nchi ilikuwa haijafikiwa na dawa za viwandani; mwingiliano wake na wenye malaria uko vipi; idadi gani ya watu wanatumia dawa zipi na waliokuwa hawatumii dawa hizo walikuwa wanatumia nini.

Kwa njia hiyo, king’ora kikilia Ulaya, kwamba sampuli ya mji mdogo kama Kongwa (Dodoma), na siyo vijijini, inaonyesha usugu wa malaria – na sehemu nyingine kama hizo katika nchi nyingine – basi inatosha kuharamisha dawa na kuingiza mpya.

Hoja ya mtanuko wa eneo la maambukizi, inakubalika; lakini kuna hoja kinzani kwamba walioambukizwa malaria ambako vidonge havikufika wamepona.

Kwa hiyo kuna njia nyingine isiyo rasmi ya kutibu ugonjwa huo na nchi za tropiki hazistahili kuendelea kuwa “panya wa maabara” – wa kufanyia majaribio ya dawa.

Hadi hapa tunaona ni kwa kiasi gani nchi za tropiki zilivyoendelea kucheza na mauti ndani ya nyumba wakati mkombozi yuko mlangoni.

Tafiti za dawa za asili za kutibu malaria zimekwenda goigoi sana katika Tanzania na nchi za tropiki, hasa Afrika wakati watafiti walikuwa na mahali pa kuanzia.

Waliougua malaria wapo. Dawa zilizotumika kuwatibu zipo. Waliotibiwa kwa mitishamba hadi wakapona wapo – ni mamilioni. Ugumu umekuwa wapi?

Hata wakati nchi za tropiki zikiendelea na utafiti na “ombaomba,” uko wapi mkakati wa kuhimiza wananchi kutumia dawa za asili?

Misitu na vichaka vya nchi za tropiki ni mali, ni dawa, ni baraka. Majani na mizizi kutoka nchi hizi, na hasa Afrika, vimetumika kutengeneza dawa ambazo zinaletwa nchini na kuuzwa aghali.

Mchungaji Emmanuel Mwakalinga wa Tukuyu, mkoani Mbeya pamoja na kazi zake za kuhubiri neno la Mungu, anatoa dawa aina mbalimbali kwa magonjwa kadha wa kadhaa.

Kwa Mwakalinga ndiko chimbuko jingine la dawa za kutibu malaria, homa ya matumbo na magonjwa mengine yaliyoshindikana. Ni dawa za mitishamba. Wako wengi wa aina hii nchi nzima na katika nchi za tropiki.

Swali kuu ni wataalam wa nchi hizi wamefanya nini, kwa miaka 50, kutumia ujuzi wa waendesha tiba kwa kutumia dawa asilia?

Serikali za nchi hizi zimefanya nini katika kujenga mazingira na kuchochea elimu katika medani hii ili kukabiliana na mbu na malaria?

Hata pale serikali ziliposhindwa kufanya haya, zimechukua hatua gani kuhimiza wananchi kutumia mitishamba iliyoko karibu nao, kwa maelekezo madogo tu ya wenye ujuzi, ili kukabili malaria?

Ninafahamu nyumba moja jijini Dar es Salaam ambayo mazingira yake yamepandwa miti shamba kwa ajili ya matibabu ya malaria.

Mjini Morogoro, kuna eneo moja karibu na viwanda, Kihonda ambako mtu mmoja amepanda miche ya mitishamba aina ya Artemisia annua. Mmea huu wenye asili ya China umekuwa ukitumiwa kwa kutibu malaria na magonjwa mengine kwa zaidi ya miaka 2000.

Pamoja na uchunguzi unaoendelea kwa ngazi ya maabara mbalimbali duniani, baadhi ya nchi za tropiki zimeanza kupanda, kuvuna na kutumia mmea huu, wenye aina zaidi ya 50, kwa tiba ya mafanikio.

Majirani wa Tanzania – Kenya na Uganda, wana bustani za mmea huu. Kenya inakadiriwa kuwa na wakulima zaidi ya 4,000 ambao wameanza kuvuna fedha kutokana na kuuza majani ya artimesia.

Asasi ya kijamii ya Natural Uwemba System for Health (NUSAG) kaskazini mwa Tanzania imekuwa ikishirikiana na asasi nyingine katika Afrika Mashariki kutafuta tiba ya malaria kwa bei nafuu na mmea huu umekuwa moja ya vyanzo vya tiba ya uhakika na isiyokuwa na athari mbaya.

Mazingira ya dawa ya sasa ya kutibu malaria ni kwamba kutokana na ughali wake, wanaofikiwa na dawa hiyo watakufa wakiitazama.

Kuna ubaya gani kwa wataalam nchini, hata kama hawajakamilisha uchunguzi wa dawa nyingi nchini zinazotibu malaria, kupiga mbiu ya matumizi ya mitishamba ambayo imelinda uhai wa mamilioni ya wananchi kwa miaka yote?

Kuna ubaya gani kufanya hoja ya kuokoa maisha ya wananchi, kwa njia ya tiba za asili, kuwa ajenda muhimu ya wataalam wa tiba na watawala?

Kuna ubaya gani kuhimiza kilimo, kikubwa na kidogo, cha Artemisia annu, hata kama sehemu ya bustani kwa kila kaya, ili watu wajiponye, angalau kwa sasa, huku wakisubiri tiba za kisasa?

Umuhimu wa kufanya haya haraka unatokana na takwimu: Mtoto mmoja hufa duniani kila baada ya sekunde 30; na kwa jumla watu milioni tatu hufa kila mwaka kutokana na malaria.

Kila kabila au jamii ina omubazi g’womushana kwa jina tofauti. Kwenye dawa hizo ongeza Artemisia annu; na nyingine na nyingine za mitishamba. Watu wapone; hata kama ni kuahirisha kifo tu.

Tuogope kutangaza tiba kwa kuwa haijafanyiwa “uchunguzi wa kisasa” au tumihimize matumizi kuokoa maisha ya watu wengi?

Sasa Mutakyahwa anatumia mitishamba kutibu malaria na ana bustani ya Artemisia annu.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii imechapishwa katika toleo la Jumatano, 17 Juni 2009 la gazeti la MwanaHALISI)

Friday, May 22, 2009

JINSI SERIKALI INAVYOTAKA KUUA UHURU WA MAONI

Serikali inavyotaka kuua uhuru wetu

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI serikali iwe kipofu au ifanywe kipofu. Kuwa kipofu ni tofauti na kutoona. Wakati kutoona ni kuondokewa na uwezo wa kuona, kuwa kipofu ni kupoteza fahamu na akili, na mara nyingi kwa kudanganywa au kwa utashi binafsi unaotokana na tamaa na, au ujinga.

Kwa mapendekezo mapya katika Sera ya Habari na Utangazaji, kwamba mtu mmoja ataruhusiwa “kumiliki aina moja tu ya chombo cha habari, kama ni magazeti, au redio au televisheni, na siyo vyote kwa wakati mmoja,” basi serikali imejitia upofu.

Kujitia upofu ni kukataa kufikiri. Ni kukata tamaa. Ni kujisalimisha kwa vihoja na viroja. Ni kushindwa kujitazama na kujitathmini. Ni kutafuta visingizio vya kuziba penye udhaifu. Ni kukoleza kulala na kusinzia kwa mishipa ya fahamu.

Kinachokoleza upofu katika mapendekezo ya marekebisho ya Sera ya Habari na Utangazaji ni maelezo ya nyongeza. Inatajwa kuwa mmiliki aliye na vyombo vyote hivyo, “apewe muda wa miaka mitano kuuza hisa za vyombo vyake vingine.”

Kwa mujibu wa muundo, kanuni na taratibu nchini, vinavyoitwa vyombo vya umma, hakika ni vyombo vya serikali. Uanzishwaji, uendeshaji, uwajibikaji na hata ugharimiaji wake, vyote ni kwa mfumo wa kumilikiwa na serikali na siyo “umma.”

Mateka wa kwanza basi sharti awe serikali ambayo kwa jina la “umma” inamiliki redio, televisheni na magazeti. Huu ndio mgongano wa kwanza wa maslahi katika utekelezaji kwa upande wa serikali.

Kwa takribani miaka 24 sasa, baadhi yetu tumetaka serikali iachie vyombo vya habari inavyomiliki ili iandikwe na kutangazwa kama inavyoonekana na siyo kwa kurembwa, kuonewa haya au inavyotaka. Serikali imekataa.

Tumependekeza serikali ijiondoe katika umiliki wa vyombo vya habari ndipo itapata hadhi na uhalali wa kuvisema na kuvikosoa, badala ya mtindo wa sasa ambapo serikali ni mshindani kama wengine lakini inatumia nafasi yake kukandamiza mshindani mwenzake.

Serikali imekataa yote hayo. Imebaki mmiliki wa vyombo vya habari; msajili wa vyombo vingine vya habari, mtunga sera, msimamizi wa sera, mdhibiti wa vyombo vya habari na bado mshindani miongoni mwa wenye vyombo vya habari. Mgongano wa maslahi.

Bali kwa uzoefu wa ukaidi wa serikali, hatutaona ikiuza redio, televisheni au magazeti yake. Tutashuhudia shinikizo kwa wenye vyombo kuuza vyombo vyao.

Mapendekezo ya sera ndiyo huzaa sera na hatimaye kuelekeza mfumo wa sheria. Marekebisho yanayopendekezwa kwenye sera ya mwaka 2003 yanaonekana yamelenga mtu mmoja au wawili wenye kumiliki aina nne za vyombo vya habari – redio, televisheni, magazeti na shirika la habari.

Hata hivyo, katika haraka ya serikali ya kudhibiti iliowalenga, haitaji Shirika la Habari kuwa aina nyingine ya chombo cha habari katika kifungu 2.3.2 kinachosomeka, “Maelekezo ya Sera.”

Wenye aina tatu za vyombo vya habari ambao serikali inaweza kuwa imelenga, ni Reginald Mengi, Mwenyekiti Mtendaji wa makampuni ya IPP na Media Solutions anayemiliki redio, televisheni na msululu wa magazeti, baadhi yakiwa na msimamo mkali wa kukosoa na kuibua taarifa za rushwa na ufisadi.

Mwingine mwenye aina tatu za vyombo vya habari ni Anthony Diallo, mmiliki na Mtendaji Mkuu wa Sahara Communications yenye redio, televisheni na gazeti moja.

Katika siku za hivi karibuni ni Reginald Mengi ambaye amelalamikiwa na serikali kwa kuipa nguvu hoja ya ufisadi nchini. Ameibuka na majina ya watu watano aliowaita “mafisadi papa.”

Hoja ya Mengi ilipojibiwa na mmoja wa waliotuhumiwa, Rostam Aziz, naye Waziri wa Habari George Mkuchika akaibuka na kudai kufunga mjadala huo kwa madai kuwa unataka “kuligawa taifa.”

Vyombo vya habari vya IPP na Media Solutions, hasa magazeti – This Day, KuliKoni na Nipashe – vimejizolea tuzo katika ushindani wa kuandika habari za uchunguzi katika rushwa na utawala bora.

Aidha, ni vyombo vya IPP, hasa televisheni, ambayo imemulika hata kelele za chinichini na mikwaruzo kati na baina ya wabunge na kutoa mwanya kwa wengi kujieleza, ambao bila chombo hicho, wangepotea kimyakimya kutoka jukwaa la siasa.

Mapendekezo ya serikali basi, yanalenga kuzima nguvu ya vyombo hivyo; mvumo na mfumo wake ratibishi na hatimaye kurejesha taifa katika usiku wa giza nene la upungufu na hata ukosefu wa taarifa ambazo, bila vyombo hivyo zisingepatikana.

Serikali inalenga kuua stadi na uwezo wa viwango ainaaina wa watumishi katika vyombo hivi; kwani pamoja na kupendekeza kuwa wenye aina zote tatu wauze hisa za aina nyingine mbili za vyombo vya habari, hakuna mwenye hakika ya vyombo vilivyouzwa kuendelea kukua, kushamiri na kutumika kwa malengo na manufaa yaliyotarajiwa.

Hapa kuna mkakati wa kuua ajira ya mamia, kama siyo maelfu ya wafanyakazi wanaotegemea vyombo hivi na wengi wanaotegemea mafao yatokanayo na mishahara ya watumishi katika vyombo hivi.

Mapendekezo ya serikali katika sera yanalenga kuzima ujasiri katika uandishi wa habari za uchunguzi; ujasiri uliopatikana baada ya muda mrefu wa mafunzo darasani na kwa njia ya vitendo.

Haya ni mapendekezo maalum ya kuzima ushindani wa kibiashara kati ya vyombo vya habari vya serikali na vyombo binafsi na kurejesha wananchi katika mazingira ya kutokuwa na utashi juu ya chombo gani wanataka kiwape habari na taarifa.

Mapendekezo yanalenga kukatisha tamaa na kuogofya wale ambao tayari walikuwa wamehamasika na wanataka kuanzisha vyombo vingine vya habari.

Hatua ya serikali kupitia mapendekezo, inalenga kupunguza kiwango cha taarifa zilizokuwa zinawafikia wananchi. Hii ina maana ya kujenga mazingira ya uficho zaidi kwa serikali na watendaji wake. Uko wapi uwazi bila vyombo vingi vya kuuweka wazi?

Hatari kubwa ipo kwenye uhuru wa maoni. Hapo ndipo kuna janga. Kuwepo kwa vyombo vingi vya habari kunaweka mazingira ya wananchi wengi kutoa na kupata habari na taarifa; kubadilishana mawazo, kuelimishwa na kuelimishana na kuwa na maoni yao juu ya mambo mbalimbali.

Sauti nyingi za wananchi juu ya wanavyoona utawala na wanavyotaka uwe; juu ya furaha, huzuni, pongezi, malalamiko, vilio, shangwe na maafa, huweza kufika kwa wenzao na watawala kama kuna vyombo vingi vya habari.

Kupunguza idadi ya vyombo vya habari katika mazingira ya sasa, ni kutaka kuziba mifereji ya fikra na elimu; ni kutoa mwanya kwa uvumi na ujinga; ni kutaka wananchi wasikilize sauti moja kutoka kileleni; ni kuzika wananchi wakiwa hai katika mazingira ambamo hawatasikika wakipambana au wakilia na kuomba msaada.

Turudi darasani kidogo na kwenye uzoefu. Uhuru wa maoni kwa maana ya uhuru wa kujieleza, haukamiliki mpaka mtu aseme maoni yake – kwa kauli au vitendo.

Ni mpaka maoni yake yasikike kwa mwenzake, kundi au halaiki; au yachapishwe kwenye gazeti, au yatangazwe kwenye redio au televisheni. Vyombo vya habari ndivyo husaidia kukamilika kwa takwa la uhuru wa maoni na ndio maana vyombo hivyo ni sehemu ya uhuru wa kujieleza.

Sasa serikali inapendekeza wenye vyombo waviuze. Labda wanao wanunuzi. Wamuuzie nani ambaye ataviendesha kama vilivyokuwa vinaendeshwa. Mapendekezo haya ndiyo yanatarajiwa kuwa katika sheria mpya ya uhuru wa habari na uhuru wa kupata habari. Hii ni hatari.

Kama pendekezo la serikali litapitishwa na wadau, au litashinikizwa, sheria itakayotokana na sera hii itakuwa moja ya sheria za kishetani ambazo wadau wa habari wamepinga tangu 1985.

Bali kuna masomo mawili yanayopatikana hapa. Kwanza, pendekezo la serikali, ikiwa mdau katika huduma na biashara ya habari, linadhihirisha kuwa imeshindwa mbinu za ushindani na sasa imeamua kutumia mabavu kwa njia ya sera na sheria.

Pili, serikali imejipanga kuingilia uhuru wa wananchi wa kupata habari na kuwa na maoni. Itafanya hivyo kwa kuviondoa vyombo vya habari ambavyo tayari vilikuwa vimepenya jamii na vinakimbiliwa na wengi ili kutoa taarifa.

Mapendekezo ya serikali hayakubaliki na kila mwenye nia njema kwa taifa hili anaitaka serikali iyatupilie mbali. Inabidi hata walioyaleta wajue kuwa wao siyo wapangaji wa kudumu serikalini. Zimwi wanalojaribu kuumba watalikuta nje ya lango pindi wakiachishwa, wakifukuzwa kazi au wakistaafu.

Serikali ingejizolea heshima kwa kuhimiza watu binafsi na asasi mbambali kuanzisha magazeti mengi na vituo vingi vya redio na televisheni, bila kujali nani ana vyombo vya aina zipi. Kinachohitajika ni taifa linaloongea; na siyo la watu walionyang’anywa uwezo wa kuwa na maoni na vyombo vya kutolea maoni hayo.

Hivi kwa nini mtu akatae kujiandalia mazingira mazuri ya uhuru uliotamalaki na badala yake ajiandalie mahabusi akingali madarakani? Tusikubali vipofu wajinyonge. Tuwanyang’anye kitanzi.



0713 614872
ndimara@yahoo.com

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, toleo la 24 Mei 2009)

Saturday, May 16, 2009

SERIKALI IKITENDA JINAI, WANANCHI WAFANYEJE?


WAZIRI MKUCHIKA (pichani juu) ATAKA KUNYAMAZISHA WANANCHI

Na Ndimara Tegambwage

SERIKALI imeficha ukweli. Katika hatua hii, serikali inaweza kutuhumiwa kusema uwongo; na kusema uwongo ni kutenda jinai. Je, serikali ikitenda jinai itakuwaje?

Katika taarifa yake, serikali imepiga marufuku kile ilichoita “malumbano” kati ya Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Reginald Mengi na Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz kwa maelezo kuwa “yanaweza kutumbukiza taifa katika uvunjaji amani.”

Taarifa ya Waziri wa Habari, George Mkuchika kwa vyombo vya habari juzi Jumatatu imesema serikali “haitakubali kusikia malumbano” hayo na “haitavumilia kuona vyombo vya habari vikichangia kuligawa taifa katika makundi na kudumaza maendeleo.”

Hapa ndipo penye mgogoro. Wasomaji wa magazeti, wasikilizaji redio na watazamaji wa televisheni hawajawahi kuona kile serikali inachokiita “malumbano.”

Mengi ametuhumu watu kuwa “mafisadi.” Mmoja wao ni Rostam. Naye Rostam amejibu, tena kwa kutumia chombo cha umma – Televisheni ya Taifa (TBC1).

Kwa akili ya kawaida, kilichotendeka ni kuibua hoja zilizokuwa zikienda chinichini. Kilichoanikwa ni matendo ya watu binafsi yanayohusu uchumi na maisha ya wananchi.

Kile ambacho serikali inaita “malumbano” ni eneo la “soko huria” la mawazo ambamo, kwa miaka miwili sasa, wananchi wamekuwa wakichangia kwa njia ya kulalama kwamba keki ya taifa inaliwa na wachache.

Sasa serikali inasema “haitakubali kusikia” na wala “haitavumilia” kuona vyombo vya habari na waandishi wakichangia kugawa taifa.

Huu ndio udikiteta mchafu. Kwanza, serikali inatafuta nini katika “malumbano?” Kama ni malumbano kweli, si iwaache walumbanao wafanye wafanyavyo? Malumbano si huisha hoja zikiisha?

Pili, serikali inajikoroga. Upande mmoja inasema kuna malumbano kati ya watu wawili; na upande mwingine inasema wananchi wameanza kugawanyika; hawa wakiunga mkono Mengi na wale wakiunga mkono Rostam.

Basi haya siyo malumbano. Huu ni mjadala wa hoja za kina. Ni mdahalo wa gonga nikugonge wa kuibua mazito na machungu yanayohusu jamii. Ni uwanja wa kumwaga taarifa kwa wenye macho kuona na wenye masikio kusikia. Ni kitanzi pia cha wasema uwongo.

Lakini serikali inasema sasa basi! Nyamaza! Huu ni ukatili. Ni udikiteta. Kuna hasara gani kwa wananchi kuwa upande wanaotaka, wanaoelewa, wanaothamini na waliotayari kutetea?

Tatu, serikali haisemi ukweli pale inapodai kuwa nchi itaingia katika “uvunjaji” amani. Watu huru wanapojadili yanayowahusu wao na jamii yao, haitazamiwi serikali ijenge visingizio vya kupotea kwa amani.

Watu wakiona mabaya yanatendeka; wakakaa kimya au wakanyamazishwa, wakajenga chuki kimyakimya, wakafura kwa hasira; basi linalofuata ni mlipuko mkubwa kuliko mabomu ya Mbagala.

Mlipuko huu ni hatari zaidi, hata na hasa kwa watawala, kuliko mdahalo juu ya nani “anakula nini.” Bali sasa ni wazi kwamba kwa hatua ya serikali ya kuzima mjadala, lazima “kuna jambo.”

Nne, serikali makini ingefurahia mdahalo. Ingepata vyanzo vizuri na sahihi vya taarifa mwanana za kufanyia kazi iwapo ina nia kweli ya kufanya kazi. Lakini inaonekana imechoka haraka na mapema.

Sasa siyo tu serikali haitaki kusikia, bali pia haitaki wananchi wasikie na washiriki mjadala. Huu ni udikteta mchafu.

Mtu angetarajia “mapapa” watajwe na “fisadi nyangumi” watajwe ili wananchi waone tofauti kati ya papa na nyangumi. Waone nani anaamsha hisia zao ili waone na kupigania haki na maisha yao.

Hakika, mmoja wa samaki hawa wakubwa aweza kuwa mwandani wa wananchi. Panahitajika uibuaji taarifa. Upembuzi. Uchokonozi wa kina na ushiriki wa wananchi katika mjadala. Kuzima hili ni ukatili wa kidikteta.

Tano, serikali inatumia vitisho kuzima mjadala. Inanukuu na kujivunia sheria katili zenye harufu ya kifashisti kama hii Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 na nyingine yenye chembechembe za kibedui – Sheria ya Utangazaji ya mwaka 2003.

Katikati ya majigambo ya utawala bora, ukiona bado kuna watawala wanaojivunia sheria zinazopingana hata na katiba zao, na uhuru na haki za wananchi, basi ujue udikteta umeota mvi. Wanaua uhuru na haki ili watawale misukule na siyo watu wanaofikiri na wenye utashi.

Sita, kwa serikali “kutahadharisha” wahariri na waandishi, ina maana ya kuwafunga midomo na mikono. Wasifikiri. Wasitende. Wasubiri serikali iamue andika hili, andika lile.

Saba, kuna upandikizaji woga. Waziri anasema sheria “zinakataza mtu, watu kuzungumzia au kujadili suala ambalo tayari liko mahakamani.” Hakuna sheria ya aina hiyo.

Chukua maneno ya waziri kama yalivyonukuliwa hapo juu. Ama waziri hakuelewa sheria inasemaje au ameinukuu nje kabisa ya muktadha. Sheria aina hiyo itakuwa za kishetani.

Magwiji wa sheria waliishafundisha kuwa waamuzi wa kesi mahakamani siyo hakimu au jaji peke yake. Kuna wakili wa pande mbili na kuna wananchi wanaofuatilia kesi.

Kila fungu litatoa hukumu yake; na hilo ndilo hufanya hakimu au jaji awe makini akijua siyo mwamuzi pekee, hata kama waamuzi wengine hawakuketi mbele ya mahakama.

Kwa hiyo suala la kutojadili kilichoko mahakamani ni uzushi unaolenga kutisha na kunyamazisha wananchi. Hata kuibuliwa kwa madai ya nyongeza, nje ya yale ambayo mtuhumiwa tayari amesomewa mahakamani, siyo kosa.

Ni kweli kabisa maoni nje ya mahakama yaweza kusaidia kuweka wazi zaidi kinachoendelea mahakamani. Hiyo ni kama mawakili watakuwa wamepata taarifa zaidi za kunoa stadi kuchokonolea kile ambacho walikuwa hawakukiona na kukiwasilisha kwa ustadi zaidi.

Lakini mjadala nje ya mahakama hauwezi, hata kidogo, kuharibu kinachoendelea mahakamani. Vitisho kama vile vya Mkuchika ndivyo vinaweza kuharibu mbongo za watu na kuwapokonya uhuru wa maoni. Naomba kuwasilisha.

Kwa hiyo, serikali imetumia mabavu kujaribu kuzima mjadala ambao ungeisadia. Sasa kuna madai kuwa imefanya hivyo kwa kuogopa itaguswa pale – kati ya papa na nyangumi.

Kuna kila sababu ya kupinga udhalimu huu katika nyakati tulizomo. Tukinyamaza watawala watashindilia watu kwenye magunia kama dagaa na kututupa mwaloni.

Kuvunjika kwa amani ni visingizio. Kutumia visingizio kukwepa ukweli ni kuficha ukweli hadi kufikia viwango vya kusema uwongo.

Kusema uwongo kuwa mjadala utaleta maangamizi kitaifa ni kutenda jinai.
Serikali ikitenda jinai wananchi wafanyeje?

0713 614871
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la 13 Mei 2009)

WANAGAPI WATAPIMWA AKILI TANZANIA?

Vimbwanga vya Ikulu, BoT na walinzi

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI kupuuza vimbwaga. Vina maana yake katika mazingira maalum ya utawala uliopo. Ilitokea katika historia ya nchi hii, moto ukaunguza Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Wengi walistuka. Wengine walishangaa. Wengi walihisi kulikuwa na njama za kuficha wizi au kuharibu ushahidi kwa kuchoma nyaraka. Ndani ya benki maofisa walikanuliana macho na kauli za “sihusiki” zikawa salaam za kila siku.

Kilichostua wengi wakati huo na hadi sasa ni aliyeshitakiwa. Alikuwa mlinzi – korokoroni. Kesi ilinguruma. Ulijengwa ushahidi wa kushindilia na kuokoa. Hukumu hii hapa. Ni mbele ya jaji.

Jaji anachukua hukumu iliyoandikwa. Anageuzageuza kurasa. Anateremsha miwani yake ambayo inagota kwenye pua. Anawaangalia waliofurika mahakama kwa kupitia juu ya miwani yake. Anawaangalia washitakiwa. Anaanza kusoma hukumu.

Ni maneno mengi. Ni sentensi nyingi. Ni aya nyingi kwenye karatasi nyingi. Mahakama imetulia, tuli! Anasoma. Anahoji na kujijibu. Anatulia kwa sekunde kadhaa na kuvuta pumzi huku waliojaa mahakama wakisubiri “hukumu.”

Kwa kauli zisizo na usumbufu wa maneno marefu, magumu na ya mchanganyiko wa Kiingereza na Kilatini, ambayo hutumiwa na wanasheria wengi, jaji anasema kuwa, kila anapoangalia pale mahakamani, haoni waliotenda jinai ya kuchoma benki.

Alikuwa na maana kwamba wahusika hawakuwa mahakamani. Hawakushitakiwa. Aliyekuwa kizimbani, kwa maoni yake, uelewa na kwa mujibu wa sheria, hakuwa na hatia. Alimwachia. Mlinzi hakuelewa. Wasikilizaji walipigwa na mshangao.

Waliochoma benki hawajawahi kufikishwa mahakamani hadi leo. Hata hivyo, mabenki hayaungui kwa moto wa sigara za wapita njia na hakuna joto la kukamata watuhumiwa wengine. Labda moto huo ulikuwa mwanzo wa kindumbwendumbwe kilichoko BoT leo.

Sikiliza ya Ikulu, Dar es Salaam. Ni alfajiri au asubuhi. Ikulu kunawaka moto. Nani kaunguza makao ya rais (mara hii yumo Benjamin Mkapa)? Wengi wanastuka. Wengine wanashangaa. Wengi wanahisi kuna kilichounguzwa ili kuharibu ushahidi.

Magari ya kuzima moto ikulu hayapo. Wanaowahi kufika ikulu ni kampuni binafsi ya ulinzi na zimamoto. Lazima walinzi wa langoni wajiulize iwapo zimamoto ya “moto wa binafsi” inaweza kuzima moto wa “ofisi ya umma.”

Subiri kidogo. Wakawasubirisha. Moto haukusubiri. Hadi uamuzi unafanywa, kwamba kampuni binafsi yaweza kuzima “moto wa umma,” moto uliishatafuna vipande vya ikulu.

Hapa hakuna kesi. Wataalam wanaeleza chanzo na hakuna wa kukamata. Lakini ikulu imeungua na ikulu haziungui kwa moto wa sigara za mpitanjia. Ni vimbwanga vya Tanzania.

Wiki iliyopita mwanaume mmoja aliingia ikulu bila kubisha hodi. Akaenda hadi maeneo ya ofisi. Bila shaka akakagua au akashangaa mandhari ya ofisi kuu ya taifa. Kwani wale ndege kishingo – tausi, wanaoranda bustanini humo kila siku hulipa kiingilio?



Baada ya utalii huu wa muda mfupi, mwanaume huyo alichuma ua bustanini ikulu; labda kwa shabaha ya kutaka kuwaonyesha wenzake kuwa alikuwa ndani ya ikulu bila kukaribishwa na rais wala ofisa yeyote. Akaanza kutoka kupitia lango kuu.

Tofauti na vimbwanga vya BoT na moto wa ikulu, hiki kina manjonjo ya aina yake: Kabwela asiye na kitanda kaingia ikulu bila kikwazo. Walinzi walikuwa wapi? Mtoto wa watu kajiingilia ikulu na analo la kusimulia, nyumbani au kijiweni.

Bahati – yoyote ile – mbaya au nzuri, mwanaume huyo akadakwa langoni akiwa anatoka. “Unatoka wapi wewe? Kwanza uliingiaje mpaka kule?” Ni maswali lakini hayana uzito bali mwanaume huyo hafanyi mikwara. Anajieleza. Huko ndiko wanaita kumatwa. Sasa kuna taarifa kuwa mtu huyo apelekwe hospitali kupimwa akili.

Katika hali yakawaida, nani anastahili kupimwa? Hapa kuna kijana aliyeingia ikulu bila kelele wala mikwaruzo na alikuwa anatoka bila kubughudhi yeyote isipokuwa akiwa amebeba ua alilochuma. Huyu apimwe nini?

Pale ikulu anakaa rais wake. Wanakaa watumishi wa umma. Wapo askari wa kulinda amani na amani ni amani yake na wakaao ikulu na wengine wanaoingia. Apimwe nini?

Si angepimwa asiyejua kuwa ikulu inapaswa kuwa eneo la utalii wa watu wa nje na ndani ya nchi na kwamba ni moja ya vivutio na sehemu ya elimu kwa jamii?

Kati ya walinzi na mwanaume aliyeingia ikulu bila hodi, nani apimwe akili? Wale ambao hawakuona mtu anaingia na aliyeingia na kutoka bila kufanya baya lolote, nani hasa apimwe akili?

Kwanza ikulu imekuwa moja ya “vijiwe” maarufu. Imezungukwa na watafuta kivuli wakati wa jua kali; wauza maji, karanga na kahawa. Hivi karibuni, baada ya wakazi wakuu wa ikulu kufoka ndipo askari wakazizunguka na kufanya kamatakamata ya zimamoto.

Lakini Makamu wa Rais Mohammed Shein amestuka zaidi hivi karibuni. Anasema ofisi zimegeuzwa soko. Ni biashara “mtindo mmoja.” Wauzaji wanaingia na kutoka, utadhani kazi za serikali zimehamishiwa kwingine; kilichochukua nafasi hiyo ni uuzaji na ununuzi wa sidiria, suruali, chupi, t-sheti, blausi, mashati, vipodozi na nywele za watu wa kale!

Wangapi watapimwa akili? Yule tu aliyeingia ikulu au na walinzi wa ikulu, watumishi wote wa ikulu, wakuu wa ikulu, wafanyabiashara – wa kuuza na kununua – wa ikulu? Nani atasalia katika kupimwa akili? Wauza karanga getini?

Ukimaliza vituko vya ikulu na BoT, njoo kwenye vituko vya kupotea kwa vilaputopu. Kwa maana ya sasa, “laptop” ni kompyuta ndogo ya mkononi au mezani. Inatumika kama kompyuta yoyote ile bali ni rahisi kubeba.

Sasa sikiliza vimbwanga vya laputopu. Leo laputopu ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) imepotea. Wanasema imeibwa “kiaina.” Huyu ndiye amekabidhiwa mamlaka ya kuamua nani ashitakiwe nani asishitakiwe. Kalaputopu kage kanaweza kuwa na nini?

Leo hiihii laputopu ya Mkemia Mkuu wa Serikali imeibwa. Wanasema imeibwa “kiaina.” Huyu ndiye mkuu wa idara ya vipimo nyeti anayekimbiliwa wa mwisho kutoa uthibitisho wa lolote linalohitajika kupimwa kikemia. Kalaputopu kake kanaweza kuwa na nini?

Kaa chini utunge matukio haya kama shanga: Moto wa BoT, moto wa ikulu, mwanaume anayetokea lango kuu la ikulu akiwa na ua mkononi na kupotea kwa laputopu za watumishi wa ngazi ya juu serikalini. Kizaazaa! Nani apimwe akili? Watapimwa wangapi?

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili toleo la 17 Mei 2009)